MAULIDI NJEMA.... GOOD MAULID HOLIDAY

Hakika, hakuna jambo jema kama kufanya maadhimisho ya kuzaliwa au kufa kwa kiongozi yoyote yule wa umma, ambaye alifanya vizuri na kuisimamia haki. Na hasa awe ni kiongozi aliyewapigania watu katika kuwapeleka ndani ya njia ya kumjua ni nani hasa aliyewaumba, na ni upi hasa wajibu wao kwa huyo aliyewaumba. Ipo orodha ndefu ya wajumbe wa Mwenyezi Mungu ambao walikuwepo hapa duniani katika zama na nyakati tofauti tofauti ili kuwafikishia wanadamu mwongozo na neno la Mungu, ili wasiweze kutekwa na Ibilisi-shetani na kupotea katika njia iliyo sahihi ya kumwabudu na kumwelekea Mwenyezi Mungu. Idadi ya wajumbe (mitume na manabii) hao ni kubwa mno, lakini kwa uchache miongoni mwao ni Bwana Mussa na habari za wana wa Israel, Yesu (nabii Issa) na harakati za Injili, Ruthi na habari za watu wa Sodoma na Gomola, Nuhu na habari ya Safina, Mzee Ibrahimu na mtihani wa kumchinja mwanawe, na wengineo wengi tu na visa (matukio) vyao vya kusisimua mno. Basi waislamu wamesimama ili kumwadhimisha kiongozi wao, Mtume Muhammad, ili kuyaenzi na kuyakumbuka mambo mbalimbali juu yake. Ni jambo linalovutia mno. Lakini mjumbe huyu wa Mwenyezi Mungu kabla hajaondoka hapa duniani (kufa) aliwaachia maneno ya tahadhari wale aliokuwanao kwamba, wajichunge mno wanapofanya maadhimisho juu yake ili wasije wakapitiliza mipaka, na mwishowe hata baadhi ya vizazi vyao vije baadaye viamue kumwabudu yeye (kumwita Mungu) kama ambavyo ilivyokuwa imekwishakutokea huko nyuma kwa baadhi ya mitume na manabii ambao baada ya kufa kwao, baadhi ya wafuasi wao waliiwaadhimisha kupita kiwango hata ikawafikia baadhi yao kuwapachika U-ungu na kuanza kuwaabudu na kuwategemea kwa mambo yao yote ya kimaombi, badala ya kumtegemea yule aliyewaumba (Mungu).....

                                                  Maulidi Njema




No comments: