Ashukuriwe sana Mwenyezi Mungu, Muumba wa mbingu na ardhi na vyote vinavyoonekana kwa macho na visivyoonekana. Kwa hakika ilikuwa ni hatari kubwa! Tarehe 08/12/2013 Mpini Wa Shoka ulikuwa mmoja wa abiria waliokuwa safarini ndani ya basi hili Maridadi ukitokea Dar es salaam kuelekea mkoa wa Mtwara (Kusini mwa Tanzania). Safari yetu tuliianza mapema, majira ya kama saa 12 na robo hivi ya asubuhi kwenye stendi ya Temeke mwisho-Dar es salaam. Ikizingatiwa kwamba kwa sasa barabara kuu ya Dar-Lindi hadi Mtwara imekwishatengenezwa kwa kiwango cha lami na kubaki kipande kidogo tu cha kumalizia, tofauti na ilivyokuwa kwa miaka kadhaa ya nyuma, kwa ujumla safari yetu ilikuwa imetulia kabisa. Lakini ghafla tu majira ya saa 06:48 mchana, wakati tukiteremka kwenye mteremko mmoja mkali uliokuwa na daraja maeneo ya Mbanja, wastani wa Kilometa 5 hivi kuufikia Mji wa Lindi, gurudumu la mbele la upande wa dereva likapiga kishindo kizito ' PWAAAAAAA!!!'. Ndani ya basi, abiria wote tukakumbwa na kihoro! Hofu ikatanda kwenye kila moyo wa kila aliyekuwemo ndani ya basi! Wenye kumkumbuka yule aliyewaumba wakazipaza sauti zao kwa nguvu zao zote wakimwomba msaada! Wenye kuwaamini wanadamu wenzao kwamba wanaweza kuwasaidia, nao wakapaza sauti zao kwa kuwataja hao watu wao! Mama weeeee, na Uwiiiiii ndizo hasa zilizokuwa zimetawala kila kona! Bahati nzuri basi halikuleta 'mauzauza' sana; dereva alifanikiwa kulimiliki hadi mwendo wa kama kilometa moja hivi mbele, akalisimamisha.....

Wakwetu, unaliona gurudumu jinsi lilivyosambaratika...!





Hili ndilo basi lenyewe.





Aliyesimama ndiye dereva wa basi....





Kazi ya kubadili gurudumu ikaanza...





Abiria tukawa tumesimama pande mbalimbali za gari tukijadiliana hili na lile..... 




 

Kama kawaida safarini watoto nao huwa hawakosekani...






Hawa wanaonekana ni kama vile ni familia moja hivi, lakini yawezekana ajali hii ndiyo iliyowafanya wakae pamoja namna hii chini ya mti huu! Yawezekani huenda hata hawajuani kabisa...  






 Hili ndilo gurudumu lililobadilishwa, baada ya kutolewa lililopasuka, na kutusaidia kusafiri salama hadi Lindi, na baadaye hadi kufika Mtwara town majira ya saa 09 hivi ya alasiri. Ashukuriwe sana Muumba.


No comments: