KONGAMANO KUBWA LA WAISLAMU MJINI ARUSHA, KULAANI TUKIO LA MLIPUKO WA BOMU KANISA KATOLIKI; LALAANI NA KUONYA WALE WOTE WANAOYATUMIA MATUKIO KAMA HAYA KUINUA VINYWA NA VIDOLE VYAO KUWAELEKEZEA SHUTUMA WAISLAMU, NA KUMBE WAISLAMU HAWAHUSIKI HATA KIDOGO KATIKA MATUKIO KAMA HAYA NA MFANO WAKE, NA HASA BAADHI YA WANASIASA NA VIONGOZI WA DINI WANAOTAFUTA MBINU MBALIMBALI ZA KUJIPATIA UMAARUFU NA KUKUBALIKA KWA NGUVU KWA WAUMINI WAO…

 

JUMAPILI 26/05/2013. Viwanja vya Msikiti Mkuu-Arusha

 

Mwongozaji wa kongamano hili, Imam Hambal wa Msikiti Mkuu Arusha, akisisitiza jambo na hasa juu ya kuwataka waislamu kuwa imara na kujitambua, kwani sasa kila ubaya wowote ule unapotendeka tu ndani ya nchi ya Tanzania, basi uzushi na vidole vyote vya lawama na shutuma vinaelekezwa kwao, hata kama aliyetenda ubaya huo siyo mwislamu.




Meza Kuu ikiwa imejaa viongozi mbalimbali.



Palipo na wakubwa hapaharibiki jambo. Mmoja wa wazee wa Kiislamu, Mzee Issa Kieti, waliopewa nafasi ya kuwasalimia waliohudhuria katika kongamano hili





Mwanasheria, Khalid Kumwecha, akichambua nukuu kadhaa kutoka katika vitabu na machapisho mbalimbali ya waandishi mashuhuri duniani, na hasa wa kikristo, yanayothibitisha jinsi tukio la mlipuko wa majengo pacha nchini Marekani (September 11), lilivyotayarishwa maalumu kabisa kwa ajili ya kuuchafua uislamu kote duniani, na kuzishawishi nchi zote kupitisha sheria ya ugaidi iliyoanzishwa na taifa la Marekani, ambayo kimaantiki haina lengo lolote lile la maana, zaidi ya kuulenga tu uislamu na waislamu wake.




Sehemu ya waliohudhuria…




Mwenyekiti wa Shura ya maimam wa Arusha (Ahal Sunna Wal Jamaah) Sheikh Mohammed Ramadhani wa msikiti wa Sakina-Maziwa, akielezea umuhimu wa amani kwa watanzania wote, na jinsi uislamu kwa mujibu wa Qur’an tukufu na hadithi za mtume Muhamad unavyokataza matendo ya uuaji, uonevu, unyanyasaji na uharibifu wa mali kwa kisingizio cha namna yoyote ile. Na jinsi hata Mtume Muhammad (s.a.w) mwenyewe namna alivyoishi kwa maelewano na mashirikiano na watu wengine wasiokuwa waislamu katika enzi za zama zake.




Amir Swalahudin, kiongozi wa tabligh, naye pia alipata fursa ya kufafanua masuala kadhaa, na hasa juu ya uchochezi unaopitishwa kwa nguvu kisiasa ndani ya nyumba za kidini, ili kuuchafua na kuupaka matope uislamu, likiwemo tukio la mlipuko wa bomu kwenye Kanisa Katoliki Parokia ya Olasiti mjini Arusha, ambapo katika wiki nzima baada ya kutokea kwa tukio hilo waislamu walishambuliwa kwa maneno ya shutuma na kulaaniwa vikali waziwazi mitaani, ndani ya vyombo vya usafiri na hata kwenye maofisi ya binafsi na yale ya Serikali kwamba wao hasa ndio wanaohusika na tukio hilo, na hawafai kabisa kuwemo ndani ya jamii ya watu wa taifa la Tanzania…




Waandishi wa habari na wapiga picha nao pia walikuwepo kwa wingi. Huyu ni mmojawao, Bw. Twaha Hussein Saidi, akiwa katika harakati za kunasa picha kadhaa za matukio.





Hata viongozi wa misikiti kadhaa ya Mji wa Arusha nao pia walihudhuria kwa wingi. Hawa ni baadhi yao. Ni viongozi vijana kabisa wa msikiti wa Taqwa, uliopo katika kata ya Daraja Mbili. Kutoka kushoto ni Kawawa Mohamedy Jailosy Kawawa (Katibu wa msikiti) na Ustaadh Mohamed Ismaili Kilongo (aliyevaa kanzu), Imam msaidizi.


 

 

 

Katika kongamano hili, pia walialikwa viongozi kadhaa wa Serikali akiwemo Mkuu wa Mkoa wa Arusha Bwana Magesa Molongo, pamoja na Kamanda Mkuu wa Polisi wa mkoa wa Arusha. Lakini hata hivyo kwa bahati mbaya sana, viongozi wote hawa waliomba udhuru kwani walikuwa wameitwa katika kikao cha dharura na Waziri Mkuu Mh. Mizengo Kayanza Peter Pinda. 

Lakini hilo halikuzuia tamko la waislamu wa Mkoa wa Arusha kusomwa hadharani (likiwa limepewa baraka zote za kusomwa na Mkuu mwenyewe wa Mkoa wa Arusha, Magesa Molongo, japo yuko safarini)…

Sheikh Mustafa Kihago ndiye aliyekuwa na jukumu hilo la kulisoma tamko hilo, ambalo limelaani waziwazi tukio la mlipuko wa Kanisa Katoliki-Olasiti, Arusha, lakini likiwaonya wanasiasa na viongozi wa kidini, hasa wa kikristo kuacha kuwanyooshea vidole waislamu, kwani kwa kufanya hivyo wajue wazi wanachochea chuki, wakati ushahidi wa jambo hilo kwamba waislamu ndio waliohusika hawana. Tamko hilo lilikwenda mbali zaidi, kwa kutolea mfano wa mauaji ya kimbari ya mwaka 1994 nchini Rwanda jinsi chanzo chake kilivyoanza taratibu kwa chochoko za kutuhumiana hapa na pale, zikichochewa na wanasiasa pamoja na vyombo vya habari, na mwisho wake wanyarwanda wakafikia hatua ya juu kabisa barani Afrika, ya kuuana na kuchinjana ovyo kama kuku.




Waliohudhuria wakisikiliza kwa makini wakati tamko likisomwa na Sheikh Mustafa Kihago...  




Diwani wa Kata ya Kati mjini Arusha kupitia C.C.M, Mh. Tojo, ndiye aliyelipokea tamko hilo na kuahidi kuliwasilisha kwa mkono wake kwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha. Nyuma ya Mh. Diwani, anaonekana mpiga picha akijaribu kuchukua picha kutokea kwa juu, ndani ya jengo la Msikiti Mkuu.




Umati wa waliohudhuria, wake kwa waume, ukiondoka kwa amani katika viwanja vya Msikiti Mkuu wa Arusha, baada ya Kongamano kukamalizika

No comments: